Machapisho yanayopendwa

6/recent/ticker-posts

HISTORIA YA IBADA KWA MOYO SAFI WA BIKIRA MARIA.

 

Bikira Maria


Moyo Safi wa Maria ni moja ya ibada zinazopendwa zaidi katika Kanisa Katoliki, mara nyingi huadhimishwa pamoja na Moyo Mtakatifu wa Yesu. Ibada hii ina mizizi yake katika Maandiko Matakatifu, ambapo Moyo wa Maria unaotafakari hutajwa mara kwa mara. Kifungu kimoja maarufu ni katika Luka 2:19, ambapo imeandikwa,

"Lakini Mariamu akayaweka maneno haya yote, akiyafikiri moyoni mwake."

Kulingana na mafundisho ya Kanisa Katoliki, Maria ni Mkingiwa Dhambi ya Asili. Hii inamaanisha alitungwa bila doa la dhambi ya asili kwa maandalizi ya Umwilisho wa Yesu Kristo. Kupitia stahili zisizo na mwisho za Mwanawe, Maria alihifadhiwa dhidi ya kutenda dhambi yoyote katika maisha yake. Alibaki Bikira katika Roho na mwili, kabla na baada ya kumzaa Yesu.

Malaika Gabrieli alimsalimu Maria kuwa "Amejaa Neema" wakati wa Kumpasha Habari. Tamko hili linamaanisha kwamba Roho yake ilipambwa na fadhila zote, zawadi, na matunda ya Roho Mtakatifu tangu wakati wa kutungwa kwake. Ukamilifu huu wa neema unadaiwa kuenea kutoka moyoni mwake, ikieleweka kimwili na kiroho, na kufanya moyo wake kuwa chanzo cha usafi wake na hivyo kuitwa Moyo Safi.

Moyo Mtakatifu wa Yesu na Moyo Safi wa Maria huheshimiwa pamoja kwa sababu Kristo alichukua ubinadamu wake mtakatifu kutoka kwa Maria. Mioyo yao iliungana pale Kalvari kwa ajili ya wokovu wa wanadamu. Moyo Mtakatifu unawakilisha upendo mkali wa Kristo kwa wanadamu, mara nyingi ukidharauliwa na kutojali kwa wanadamu, wakati Moyo Safi unawakilisha upendo wa Maria kwa Mungu na hamu yake ya kuleta roho kwa Mwanawe, mara nyingi ukikosewa na dhambi za wanadamu.

Kwa karne nyingi, watakatifu na wanatheolojia walitafakari juu ya moyo wa Maria, unaotambulika katika Maandiko kwa kutafakari na kuweka kumbukumbu matukio matakatifu kutoka maisha ya Yesu. Tafakari hii ilipelekea maendeleo ya ibada kwa moyo wa Maria, sawa na ibada kwa Moyo Mtakatifu wa Yesu, ambao ulichomwa kwa mkuki msalabani. Vivyo hivyo, Moyo wa Maria, uliouchomwa kwa kuungana na Mwanawe, unatoa neema kwa kila Roho ya Mkristo.

Ibada kwa Moyo wa Maria  ilichanua hasa wakati wa zama za Kati, na Mtakatifu Yohana Eudes alieneza ibada hii kwa nguvu katika karne ya 17. Alifanya kazi ya kuanzisha sikukuu ya Moyo Safi wa Maria, kuanzia katika nchi yake ya Ufaransa. Ibada hii ilipata msukumo zaidi baada ya matokeo ya Bikira Maria  mnamo 1830 huko Paris, ambayo yalihusisha kupatikana kwa  Medali ya Miujiza.

Umaarufu wa Medali ya Miujiza ulisababisha kuundwa kwa Umoja Mkuu wa Moyo Safi wa Maria, Kimbilio la Wenye Dhambi, ulioanzishwa huko Paris mnamo 1836 na kuenea haraka kote duniani. Ibada hii ilileta neema nyingi, hasa wongofu wa wenye dhambi. Mnamo 1855, sikukuu ya Moyo Safi wa Maria iliidhinishwa na Vatikani, lakini bado haikuanzishwa kwa Kanisa la ulimwengu.

 

Matokeo ya Mama Yetu wa Fatima yaliinua ibada hii kwa kiwango kipya. Maria alionyesha Moyo wake Safi uliozungukwa na miiba, ikiashiria dhambi dhidi yake. Aliomba Urusi kuwekwa Wakfu kwa Moyo wake Safi ili kuzuia vita duniani kote. Ujumbe huu ulisisitiza umuhimu wa malipizi ya dhambi na wokovu wa roho, na ahadi ya ushindi kwa Moyo wake Safi kutambulika na Kanisa lote.

Mnamo 1944, Papa Pius XII aliweka sikukuu ya Moyo Safi wa Maria kwa Kanisa lote ulimwenguni, awali ikisherehekewa Agosti 22 lakini baadaye ikahamishiwa Jumamosi baada ya sikukuu ya Moyo Mtakatifu wa Yesu. Mabadiliko haya yalihakikisha mioyo miwili ionekane pamoja kwenye kalenda ya kiliturujia. Kanisa linahimiza ibada maalum kwa Moyo Safi wa Maria wakati wote wa mwezi wa Agosti, kuimarisha uhusiano na ibada hii pendwa ya Maria.

Post a Comment

0 Comments