Machapisho yanayopendwa

6/recent/ticker-posts

JINSI YA KUSALI ROZARI TAKATIFU NA SALA ZAKE.

 


ROZARI TAKATIFU


Rozari takatifu ni sala yenye nguvu na maarufu sana katika Kanisa Katoliki, husaliwa na wakristu kutafakari maisha ya Yesu na Maria yaani Fumbo la Ukombozi, hasa kipindi cha mwezi Mei na Oktoba. Inahimizwa kuisali kama familia kila siku. Tusali rozari tupate amani, wakosefu waongoke na wasiomjua Yesu Kristu wamjue na kuokoka.

Namna ya kusali Rozari.

Hatua ya kwanza: Anza kusali Rozari kwa kuibusu miguu ya Bwana Yesu katika picha yake Msalabani kisha fanya Ishara ya Msalaba gusisha msalaba huo kwenye paji la uso, kifuani, bega la kushoto na kwa kutumia msalaba wa Rozari takatifu huku ukiwa unasema

“Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina”.

Hatua ya pili:Taja kwa ufupi nia ulizonazo. Tangaza nia hizo kwa sauti kama mnasali wengi kwa pamoja, Mfano, unaweza kusema

“Tusali kuombea amani katika nchi yetu na ulimwenguni kote" au tutolee rozari hii kuwaombea wagonjwa wetu: au :tuwaombee wote walioomba tuwaombee" nk. Hiyo ni mifano tu.”

Au unaweza kutoa mambi kuendana na tendo lililotangazwa kwenye fungu husika la tendo la rozari, au namna nyingine itakayofaa.

Hatua ya tatu: Baada ya kufanya Ishara ya msalaba na kutoa nia za Rozari yako, Sali sala ya Kanuni ya Imani:

Nasadiki kwa Mungu, Baba Mwenyezi, mwumba mbingu na dunia. Na kwa Yesu Kristu, Mwanaye wa pekee, Bwana wetu; aliyetungwa kwa Roho Mtakatifu, akazaliwa na Bikira Maria, akateswa kwa mamlaka ya Ponsyo Pilato, akasulubiwa, akafa, akazikwa, akashukia kuzimu; siku ya tatu akafufuka katika wafu; akapaa mbinguni; amekaa kuume kwa Mungu Baba Mwenyezi; toka huko atakuja kuwahukumu wazima na wafu. Nasadiki kwa Roho Mtakatifu, Kanisa takatifu katoliki, ushirika wa Watakatifu, maondoleo ya dhambi, ufufuko wa miili, uzima wa milele. Amina

Hatua ya nne:  Baada ya kusali Kanuni ya msalaba, kwenye punje kubwa ya Rozari inayofuata Sali sala ya Baba yetu:

Baba Yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe; ufalme wako ufike, utakalo lifanyike, duniani kama mbinguni. Utupe leo mkate wetu wa kila siku, utusamehe makosa yetu, kama tunavyowasamehe na sisi waliotukosea. Usitutie katika kishawishi, lakini utuopoe maovuni. Amina

Hatua ya tano: Baada ya Sala ya Nasadiki pamoja na ya Baba Yetu,  katika punje tatu za Rozari zinazofuata tunamwomba Mungu (Utatu Mtakatifu) fadhila za Imani, Matumaini na Mapendo, zikiambatana na Salamu Maria tatu.

Mojawapo ya maneno yafuatayo hutumika:


“Mungu Baba utuongezee Imani.

Salamu Maria, umejaa neema, Bwana yu nawe. Umebarikiwa kuliko wanawake wote. Na Yesu Mzao wa tumbo lako amebarikiwa. Maria Mtakatifu, Mama wa Mungu, utuombee sisi wakosefu, sasa na saa ya kufa kwetu. Amina.

Mungu Mwana utuongezee matumaini,

Salamu Maria, umejaa neema, Bwana yu nawe. Umebarikiwa kuliko wanawake wote. Na Yesu Mzao wa tumbo lako amebarikiwa. Maria Mtakatifu, Mama wa Mungu, utuombee sisi wakosefu, sasa na saa ya kufa kwetu. Amina.


Mungu Roho Mtakatifu washa nyoyo zetu kwa mapendo yako,

Salamu Maria, umejaa neema, Bwana yu nawe. Umebarikiwa kuliko wanawake wote. Na Yesu Mzao wa tumbo lako amebarikiwa. Maria Mtakatifu, Mama wa Mungu, utuombee sisi wakosefu, sasa na saa ya kufa kwetu. Amina.


Au;

“Utuongezee Imani ee Bwana,

Salamu Maria, umejaa neema, Bwana yu nawe. Umebarikiwa kuliko wanawake wote. Na Yesu Mzao wa tumbo lako amebarikiwa. Maria Mtakatifu, Mama wa Mungu, utuombee sisi wakosefu, sasa na saa ya kufa kwetu. Amina.


Utuongezee matumaini ee Bwana,


Salamu Maria, umejaa neema, Bwana yu nawe. Umebarikiwa kuliko wanawake wote. Na Yesu Mzao wa tumbo lako amebarikiwa. Maria Mtakatifu, Mama wa Mungu, utuombee sisi wakosefu, sasa na saa ya kufa kwetu. Amina.


Uwashe nyoyo zetu kwa mapendo yako ee Bwana,

Salamu Maria, umejaa neema, Bwana yu nawe. Umebarikiwa kuliko wanawake wote. Na Yesu Mzao wa tumbo lako amebarikiwa. Maria Mtakatifu, Mama wa Mungu, utuombee sisi wakosefu, sasa na saa ya kufa kwetu. Amina.

 

Hatua ya sita: Katika Punje kubwa inayofuata baada ya punji ndogo tatu Sali sala ya Atukuzwe Baba.

 

Atukuzwe Baba, na Mwana na Roho Mtakatifu, kama mwanzo na sasa na siku zote, na milele, Amina.

 

Hatua ya saba: Tafakari juu ya fumbo la kwanza: Kila fungu la Rozari linahusishwa na fumbo linalohusiana na maisha ya Yesu au Mama Bikira Maria. Anza na fumbo la kwanza. Tafakari juu ya fumbo hilo na kisha usali Baba Yetu kwenye punje kubwa.

Hatua ya nane: Ukiwa umeshika Rozari, sali Salamu Maria mara kumi, yaani Salamu Maria moja kwa kila  punje ndogo kumi za Rozari. Unaposali kila Salamu Maria, zingatia fumbo ulilolitaja mwanzoni na utafakari umuhimu wake unapoendelea kusali.

Hatua ya Tisa:  kwenye punje kubwa inayofuata Baada ya Salamu Maria kumi, sali Sala  Sala ya Atukuzwe Baba...... Kisha Sali sala zifuatazo:

Tuwasifu milele, Yesu, Maria na Yosefu,

Ee Yesu wangu, utusamehe dhambi zetu, utukinge na moto wa milele, ongoza roho zote mbinguni, hasa za wale wanaohitaji  zaidi huruma yako.

 

Hatua ya kumi: Taja fumbo la pili: Endelea na utaratibu kama wa hapo juu hadi kwenye fumbo lifuatalo na urudie hatua ya 7 hadi hatua ya 9.

Hatua ya kumi na moja: Endelea na mafumbo yaliyosalia: Rudia hatua ya 7 hadi 9 kwa mafumbo yaliyosalia, ukitangaza kila moja kabla ya kusali salamu Maria  Kumi.

Hatua ya kumi na mbili: Baada ya kukamilisha miongo yote mitano, maliza Rozari kwa sala ya Salamu Malkia (Salve Regina).

Salamu Malkia, Mama mwenye huruma, uzima, tulizo, matumaini yetu, Salamu!
Tunakusihi ugenini hapa sisi wana wa Eva. Tunakulilia, tukilalamika na kuhuzunika bondeni huku kwenye machozi. Haya basi Mwombezi wetu, utuangalie kwa macho yako yenye huruma, na mwisho wa ugeni huu, utuonyeshe Yesu, Mzao Mbarikiwa wa tumbo lako. Ee Mpole, ee Mwema, ee Mpendelevu, Bikira Maria.

 

Hatua ya kumi na tatu: Maliza Rozari kwa kufanya Ishara ya Msalaba na kusema, "Kwa jina la Baba, na la Mwana, na la Roho Mtakatifu. Amina.

 

MATENDO YA ROZARI

MATENDO YA FURAHA (Jumatatu na Jumamosi)


Tendo la kwanza; Malaika Gabrieli anampasha habari Maria kuwa atakuwa Mama wa Mungu.

Tumwombe Mungu atujalie unyenyekevu.


Tendo la pili; Maria Mtakatifu anakwenda kumtembelea Elizabeti.

Tumwombe Mungu atujalie mapendo ya jirani.


Tendo la tatu; Yesu anazaliwa Betlehemu.

Tumwombe Mungu atujalie moyo wa ufukara


Tendo la nne; Yesu anatolewa hekaluni.

Tumwombe Mungu atujalie usafi wa moyo.


Tendo la tano; Maria anamkuta Yesu hekaluni.

Tumwombe Mungu atujalie kuwatii wakubwa wetu.

 

MATENDO YA UCHUNGU (Jumanne na Ijumaa).


Tendo la kwanza; Yesu anatoka jasho la damu kwa ajili yetu.

Tumwombe Mungu atujalie sikitiko la dhambi.


Tendo la pili; Yesu anapigwa kwa mijeledi kwa ajili yetu.

Tumwombe Mungu atujalie kuacha dhambi za uchafu.


Tendo la tatu; Yesu anatiwa miiba kichwani kwa ajili yetu.

Tumwombe Mungu atujalie kushinda kiburi.


Tendo la nne; Yesu anachukua Msalaba kwa ajili yetu.

Tumwombe Mungu atujalie kuvumilia taabu.


Tendo la tano; Yesu anakufa Msalabani.

Tumwombe Mungu atujalie kuwapenda Yesu na Maria.

MATENDO YA UTUKUFU (Jumatano na Jumapili)


Tendo la kwanza; Yesu anafufuka.

Tumwombe Mungu atujalie kugeuka watakatifu.


Tendo la pili; Yesu anapaa mbinguni.

Tumwombe Mungu atujalie kwenda mbinguni.


Tendo la tatu; Roho Mtakatifu anawashukia Mitume.

Tumwombe Mungu atujalie bidii katika dini yetu.


Tendo la nne; Bikira Maria anapalizwa mbinguni.

Tumwombe Mungu atujalie kufa vizuri.


Tendo la tano; Bikira Maria anawekwa Malkia mbinguni.

Tumwombe Mungu atujalie kudumu katika njia njema.



MATENDO YA MWANGA (Alhamisi)


Tendo la kwanza; Yesu anabatizwa Mto Jordani.

Tumwombe Mungu atujalie uaminifu kwa ahadi zetu za ubatizo.


Tendo la pili; Yesu anageuza maji kuwa divai huko Kana.

Tumwombe Mungu atujalie kuukoleza ulimwengu kwa chachu ya injili.


Tendo la tatu; Yesu anatangaza Ufalme wa Mungu.

Tumwombe Mungu atujalie kupokea Ufalme wake kwa toba ya kweli.


Tendo la nne; Yesu anageuka sura.

Tumwombe Mungu atujalie neema ya kuung’arisha ulimwengu kwa uso wa Yesu.

Tendo la tano; Yesu anaweka Sakramenti ya Ekaristi.

Tumwombe Mungu atujalie neema ya kujitoa sadaka kwa ajili ya wengine.

LITANIA YA BIKIRA MARIA.

Bwana utuhurumie
Bwana utuhurumie
Kristo utuhurumie
Bwana utuhurumie
Bwana utuhurumie
Kristo utusikie
Kristo utusikilize
Mungu Baba wa Mbinguni,……                                  Utuhurumie
Mungu Mwana Mkombozi wa dunia ………                Utuhurumie
Mungu Roho Mtakatifu ……..                                    Utuhurumie
Utatu Mtakatifu Mungu Mmoja ……..                       Utuhurumie
Maria Mtakatifu ……….                                               utuombee
Mzazi Mtakatifu wa Mungu ……..                             utuombee
Bikira Mtakatifu Mkuu wa Mabikira ……..                utuombee
Mama wa Kristo ………                                               utuombee
Mama wa Neema ya Mungu …………..                     utuombee
Mama Mtakatifu sana ………                                      utuombee
Mama mwenye usafi wa Moyo ………..                    utuombee
Mama mwenye ubikira ………..                                  utuombee
Mama usiye na doa ………..                                       utuombee
Mama mpendelevu ……….                                        utuombee
Mama mstajabivu ……….                                           utuombee
Mama wa Muumba ……….                                         utuombee
Mama wa Mkombozi …………..                                  utuombee
Mama wa Kanisa………..                                             utuombee
Bikira mwenye utaratibu …………..                            utuombee
Bikira mwenye heshima …………..                             utuombee
Bikira mwenye sifa …………..                                     utuombee
Bikira mwenye uwezo …………..                                utuombee
Bikra mweye huruma …………..                                 utuombee
Bikra mwaminifu…………..                                          utuombee
Kioo cha haki …………..                                               utuombee
Kikao cha hekima …………..                                      utuombee
Sababu ya furaha yetu …………..                               utuombee
Chombo cha neema …………..                                   utuombee
Chombo cha kuheshimiwa …………..                        utuombee
Chombo bora cha ibada …………..                            utuombee
Waridi lenye fumbo …………..                                    utuombee
Mnara wa Daudi …………..                                          utuombee
Mnara wa pembe …………..                                        utuombee
Nyumba ya dhahabu …………..                                  utuombee
Sanduku la Agano …………..                                      utuombee
Mlango wa Mbingu …………..                                     utuombee
Nyota ya asubuhi …………..                                        utuombee
Afya ya wagonjwa …………..                                      utuombee
Kimbilio la wakosefu …………..                                  utuombee
Mtuliza wenye huzuni …………..                                 utuombee
Msaada wa waKristo …………..                                  utuombee
Malkia wa Malaika …………..                                      utuombee
Malkia wa Mababu …………..                                      utuombee
Malkia wa Manabii …………..                                      utuombee
Malkia wa Mitume …………..                                       utuombee
Malkia wa Mashahidi …………..                                  utuombee
Malkia wa Waungama dini …………..                         utuombee
Malkia wa Mabikira …………..                                     utuombee
Malkia wa Watakatifu wote …………..                        utuombee
Malkia uliyepalizwa Mbinguni …………..                   utuombee
Malkia wa Rozari takatifu …………..                           utuombee
Malkia wa amani …………..                                         utuombee
Mwanakodoo wa Mungu uondoaye dhambi za ulimwengu,…   Utusamehe ee Bwana.
Mwanakondoo wa Mungu uondoaye dhambi za ulimwengu,…. Utusikilize ee Bwana
Mwanakondoo wa Mungu uondoaye dhambi za ulimwengu,..  Utuhurumie.


Utuombee, Mzazi Mtakatifu wa Mungu,…………..Tujaliwe ahadi za Kristo.


Tuombe
Ee Bwana Mungu, utujalie sisi watumishi wako afya ya roho na mwili siku zote; na kwa maombezi matukufu ya Maria Mtakaatifu Bikira daima, tuopolewe na mashaka ya saa, tupate na furaha za milele. Kwa Kristo Bwana wetu.AMINA

KUMBUKA.

KUMBUKA EE Bikra Maria mpole sana, haijasikika kamwe kwamba ulimuacha mtu aliyekimbilia ulinzi wako, aliyeomba msaada na maombezi yako. Kwa matumaini hayo, nakukimbilia, ee mama mkuu wa mabikra nakuja kwako nasimama mbele yako,nikilalamika mimi mkosefu, ewe mama wa Neno wa Mungu, Naomba usikatae maneno yangu,bali uyasikilize. AMINA.

 



 

Post a Comment

0 Comments