Machapisho yanayopendwa

6/recent/ticker-posts

IBADA YA KULIPIA YA IJUMAA TISA ZA KWANZA ZA MWEZI KWA MOYO MTAKATIFU WA YESU

 

Moyo Mtakatifu wa Yesu


Mwisho wa karne ya 17, Bwana Wetu alimtokea Mtakatifu Margaretha Maria Alakoki (1647-1690) na kumwomba aeneze Ibada kwa Moyo Wake Mtakatifu. Katika barua aliyomwandikia Mkuu wa Shirika lao mwezi Mei 1688, Mtakatifu Margaretha Maria alimueleza kuhusu kile kinachoitwa “Ahadi Kuu ya Bwana Wetu” kwa wale watakao fanya Ibada ya kulipia kila  Ijumaa ya Kwanza ya mwezi kwa miezi tisa mfululizo pia Bwana wetu alimwambia juu ya nini tunapaswa kufanya ili kuipata ahadi hiyo, Bwana wetu alimwambia Mtakatifu Maria Alakoki:

“Kwa sababu ya huruma kubwa mno ya Moyo wangu nakupa ahadi, ya kwamba mapendo yangu yenye enzi yatawapa wote wenye kupokea komunio Takatifu Ijumaa ya kwanza ya mwezi kwa miezi tisa mfululizo neema ya kutubu saa ya mwisho; hawatakufa katika hasira yangu, wala bila sakramenti; Moyo wangu wa kimungu utakuwa kimbilio lao katika kufa kwao.”

Sasa baada ya kusikia Habari ya ahadi kubwa. Najua utakuwa unajiuliza: “Nifanye nini, ili nipate mazao ya ahadi hiyo kubwa?”.

Kwanza kila mmoja, apendaye kushirikiana katika mazao hayo ya ajabu hana budi kuipokea komunio ya kutuliza Ijumaa ya kwanza ya mwezi kwa miezi tisa mfululizo.

Watu wengi wataona shida sana kushika ijumaa tisa za kwanza. Lakini hilo litawezekana tu iwapo ukifanya juhudi kubwa. Lakini bora ufanye juhudi kubwa, kwani hata katika hali ya kawaida unapotaka kununua kitu cha thamani kubwa ni lazima ufanye kazi kwa bidii ili upate pesa kwa ajili ya kununua kitu hicho. Basi ukitaka kupata ulinzi wa pekee wa Mungu saa ya kufa na matumaini makubwa ya kuingia katika uzima wa milele, hutalegea kufanya juhudi kubwa. Utakuwa tayari kuzishinda shida na kulipa kwa sadaka zako . hutaogopa mvua, wala taabu yoyote, bali utafurahi kujitolea sadaka. Utamkumbuka Yesu aliyekwenda njia ya msalaba siku ya ijumaa kuu, nawe utatamani kumfuata kwa mapendo. Siku za kutimiza masharti ya kupata mazao ya ahadi kubwa utajaa furaha na tulizo.

Moyo Mtakatifu wa Yesu ni mwema mno. Nao hufurahishwa pia na komunio ya kutuliza ipokewayo  siku ya Dominika. Tena Yesu atawalipa wenye kuipokea siku hiyo, kwa maana hisani yake haina mipaka. Lakini ukitaka kuyapata mazao ya ahadi kubwa kwa hakika, huna budi kupokea komunio Takatifu ijumaa ya Moyo Mtakatifu wa Yesu, yaani siku iliyowekwa na Bwana Yesu mwenyewe.

Hata kama mtu ameanza kuzishika Ijumaa tisa za kwanza na amekosa nafasi ya kupokea Komunio Takatifu Ijumaa moja ya katikati, hana budi kuanza upya tena.

Ila watu wasiopata nafasi yoyote kuzishika Ijumaa, waipokee Komunio ya Kutuliza Dominika badala yake. Nao waitumaini hisani ya Bwana Yesu atakayewagawia katika wingi wake.

Pili, wenye kushika Ijumaa tisa za Moyo Mtakatifu wa Yesu hawana budi kupokea Komunio Takatifu katika hali nzuri tena kwa kusudi lililotajwa na Yesu, yaani kufurahisha Moyo wake Mtakatifu, na kuulipa makosa ya watu. Basi ukitaka kuyapata mazao ya ahadi kubwa, usisahau  kufanya maungamo kwa padre na kuweka kusudi hilo kabla ya kupokea komunio ya kutuliza.

Pia unaweza kusali sala ifuatayo baada ya kupokea komunio ya kutuliza:

Ee Yesu, wewe u rafiki yangu na mkombozi wangu. Lakini ole wangu, nilifanya nini? Nilikudharau Mara nyingi. Nilikuwa kama kibarua anayengoja amri tu bila bidii yake mwenyewe. Hata amri  zako nilizishika nusu tu. Nawe umeningojea kwa uvumilivu. Leo unaniita tena nikupende vile rafiki anavyompenda rafiki.

Toka leo nitaitikia mapendo yako kwa mapendo. Kwa hiari yangu nitshika ijumaa ya Moyo Mtakatifu wa Yesu. Nitapokea komunio takatifu siku hiyo, ili niufurahishe Moyo wako na kulipa makosa unayokosewa na watu.

Kabla ya kupokea komunio ya kutuliza nitaweka kusudi hili:

“Bwana wangu, sasa nataka kupokea Komunio Takatifu, ili nikurudishie mapendo na kukufariji kwa ajili ya ubaridi wote na dhambi zote ulizokosewa na watu katika sakramenti ya mapendo.”

Ee Yesu nakuomba, unipe nguvu nishike kusudi hilo. Nami najua ya kuwa wewe utashika maneno yako uliyomwambia Mtakatifu Margareta Maria, ndiyo: “ Nitakuwa kimbilio lako katika Maisha na hasa saa ya kufa”.

Moyo wa Yesu, matumaini yao wanaokufa katika neema yako, utuhurumie.

Moyo wa Yesu, malipo kwa dhambi zetu, utuhurumie.

 

Post a Comment

0 Comments