Je ni
kweli kuwa wakatoliki Tunamwabudu Bikira Maria? Kwa kusema wazi, hapana,
hatumwabudu; tunamheshimu Bikira Maria. Kuna aina tatu za Ibada katika Kanisa
Katoliki: Latria, Dulia na Hyperdulia. 'Dulia' ni heshima inayotolewa
kwa watakatifu. 'Hyperdulia' inamaanisha heshima kubwa, inayotolewa kwa Bikira
Maria pekee, na 'Latria' inamaanisha ibada, au kuabudu, inayotolewa kwa Mungu
pekee.
Kanisa
linajumuisha sehemu tatu - kanisa la Mbinguni
(kanisa shindi), kanisa la toharani
(kanisa teswa) na kanisa la duniani
(kanisa hija), na sehemu hizi tatu zinaunganishwa kupitia sala. Kanisa la Mbinguni linatuombea sisi sote, na wakati
roho zilizo toharani zinateseka, ni kanisa duniani ambalo linawaombea wale
waliopo toharani. Hivyo, tunakuwa sehemu moja katika mwili wa Yesu Kristo.
Lakini
kwa nini tunamwomba Bikira Maria atuombee kwa niaba yetu?
Tunapofanya
Ibada kwa Bikira Maria tunamuomba atuombee kwa niaba yetu. Uombezi wa Bikira
Maria ni wenye nguvu, kwani ana mamlaka zaidi mbele za Yesu kuliko mtu mwingine
yeyote duniani, mfano mzuri ukiwa katika karamu ya arusi ya Kana, ambapo
aliombea kwa niaba ya mke na mumewe na Yesu akamsikiliza.
Yakobo
5:16 inasema, "Ungameni dhambi zenu nyinyi kwa nyinyi na kuombeana,
mpate kuponywa, kuomba kwake mwenye haki kwafaa sana, akiomba kwa bidii".
Wakati mwingine, tunapoona sala zetu hazisikilizwi, tunawaomba mapadre na wale
wanaosali kwa bidii watuombee. Kama watu wa kawaida, tunaamini kwamba mapadri,
ambao daima wako na Neno la Mungu na katika uwepo wa Mungu, ni watakatifu na
wenye haki na hivyo, tunahitimisha kwamba sala zao zitakuwa na nguvu. Katika
barua za Mtume Paulo na Mtume Petro, mitume wanawaomba wenzao wasali kwa ajili
yao kwa sababu sote ni waombezi, na hii ndiyo hasa tunayoiomba kwa Bikira
Maria, ambaye ni mwenye haki, mtakatifu na ana nafasi kubwa mbinguni.
Waprotestanti
wanaweza kuamini kwamba tunaweza kuombeana sisi kwa sisi kwa ajili yetu kwa
kuwa tu bado hai, lakini Bikira Maria, Mtakatifu Yosefu na watakatifu wote ni
wafu - basi wanaweza kutufanyia nini sasa? Biblia inasema wazi katika Luka
20:37-38 kwamba Musa anasema "Bwana ni Mungu wa Ibrahimu, wa Isaka na wa
Yakobo. Wala siyo Mungu wa wafu, bali wa walio hai; maana wote kwake hao wako
hai." Kulingana na Neno hili la Mungu, Bikira Maria yu hai na katika uwepo
wa Mungu. Ikiwa yeye na watakatifu wengine wako hai, je, wanaweza kuzungumza na
Yesu na wanayo uhusiano na Mungu? Je, wanajua kinachoendelea duniani?
Tunaposoma
kuhusu Ufufuo wa Bwana wetu juu huko Mlima Thabari katika Luka 9:29-31, tunajua
kwamba "alipokuwa akisali, umbo la uso wake likabadilika, na mavazi yake
yakawa meupe na yanang'aa. Watu wawili walionekana wakiwa wamesimama naye, Musa
na Eliya, wakiongea na kumwambia juu ya kifo chake atakachokipata
Yerusalemu." Eliya alionyeshwa kuwa mbinguni, Musa alikufa na kuzikwa,
lakini katika Injili ya Luka, waliongea na Yesu. Walikuwa na nia ya kujua
kuhusu kuondoka kwa Yesu na matukio yanayotarajiwa kutokea duniani.
Bikira
Maria, ambaye ni muhimu zaidi kuliko Musa na Eliya, anajua kinachoendelea
duniani. Amewatokea wengi, kama ilivyo katika Fatima, Misri, Mexico, Lourdes na
Rwanda, na kuwaomba watu kusali na kutubu. Ana mawasiliano ya mara kwa mara na
Yesu, Baba wa Mbinguni na Roho Mtakatifu, na ndiyo sababu tunamuomba aombe kwa
niaba yetu. Ni kwa njia ya uombezi wake wenye nguvu ndio maajabu yasiohesabika
yametokea katika maeneo yote haya, na mengi zaidi.
Kwa kuhitimisha,
Hatumuabudu Maria; sisi ni waaminifu kwake, na tunamwomba. Ana masikio ya
Mwanae Yesu na Baba yake, Mungu. Ni nani bora zaidi tunapaswa kumuomba,
kumwomba, au kutafuta uombezi wake? Yeye ni mtetezi wetu; yeye ni Mama
Mtakatifu wetu. Tunamuabudu Mungu Baba, Mwanae Yesu, na Roho Mtakatifu. Tunamheshimu
Mama yetu Mbarikiwa. Tofauti kubwa! Tunajitolea kwake kwa sababu bila yeye,
hatungekuwa na Mwanae kama Mwokozi wetu! Yeye ni mama wa Bwana wetu na, kama
hivyo, ni mama yetu. Tunamtukuza mama yetu daima, iwe ni mama wa kibinadamu au
wa kiroho!.
0 Comments