Machapisho yanayopendwa

6/recent/ticker-posts

JE WAKATOLIKI WANAMUABUDU BIKIRA MARIA?

 



Je ni kweli kuwa wakatoliki Tunamwabudu Bikira Maria? Kwa kusema wazi, hapana, hatumwabudu; tunamheshimu Bikira Maria. Kuna aina tatu za Ibada katika Kanisa Katoliki: Latria, Dulia na Hyperdulia. 'Dulia' ni heshima inayotolewa kwa watakatifu. 'Hyperdulia' inamaanisha heshima kubwa, inayotolewa kwa Bikira Maria pekee, na 'Latria' inamaanisha ibada, au kuabudu, inayotolewa kwa Mungu pekee.

Kanisa linajumuisha sehemu tatu - kanisa  la Mbinguni (kanisa shindi), kanisa la  toharani (kanisa teswa) na kanisa  la duniani (kanisa hija), na sehemu hizi tatu zinaunganishwa kupitia sala. Kanisa  la Mbinguni linatuombea sisi sote, na wakati roho zilizo toharani zinateseka, ni kanisa duniani ambalo linawaombea wale waliopo toharani. Hivyo, tunakuwa sehemu moja katika mwili wa Yesu Kristo.

Lakini kwa nini tunamwomba Bikira Maria atuombee kwa niaba yetu?

Tunapofanya Ibada kwa Bikira Maria tunamuomba atuombee kwa niaba yetu. Uombezi wa Bikira Maria ni wenye nguvu, kwani ana mamlaka zaidi mbele za Yesu kuliko mtu mwingine yeyote duniani, mfano mzuri ukiwa katika karamu ya arusi ya Kana, ambapo aliombea kwa niaba ya mke na mumewe na Yesu akamsikiliza.

Yakobo 5:16 inasema, "Ungameni dhambi zenu nyinyi kwa nyinyi na kuombeana, mpate kuponywa, kuomba kwake mwenye haki kwafaa sana, akiomba kwa bidii". Wakati mwingine, tunapoona sala zetu hazisikilizwi, tunawaomba mapadre na wale wanaosali kwa bidii watuombee. Kama watu wa kawaida, tunaamini kwamba mapadri, ambao daima wako na Neno la Mungu na katika uwepo wa Mungu, ni watakatifu na wenye haki na hivyo, tunahitimisha kwamba sala zao zitakuwa na nguvu. Katika barua za Mtume Paulo na Mtume Petro, mitume wanawaomba wenzao wasali kwa ajili yao kwa sababu sote ni waombezi, na hii ndiyo hasa tunayoiomba kwa Bikira Maria, ambaye ni mwenye haki, mtakatifu na ana nafasi kubwa mbinguni.

Waprotestanti wanaweza kuamini kwamba tunaweza kuombeana sisi kwa sisi kwa ajili yetu kwa kuwa tu bado hai, lakini Bikira Maria, Mtakatifu Yosefu na watakatifu wote ni wafu - basi wanaweza kutufanyia nini sasa? Biblia inasema wazi katika Luka 20:37-38 kwamba Musa anasema "Bwana ni Mungu wa Ibrahimu, wa Isaka na wa Yakobo. Wala siyo Mungu wa wafu, bali wa walio hai; maana wote kwake hao wako hai." Kulingana na Neno hili la Mungu, Bikira Maria yu hai na katika uwepo wa Mungu. Ikiwa yeye na watakatifu wengine wako hai, je, wanaweza kuzungumza na Yesu na wanayo uhusiano na Mungu? Je, wanajua kinachoendelea duniani?

Tunaposoma kuhusu Ufufuo wa Bwana wetu juu huko Mlima Thabari katika Luka 9:29-31, tunajua kwamba "alipokuwa akisali, umbo la uso wake likabadilika, na mavazi yake yakawa meupe na yanang'aa. Watu wawili walionekana wakiwa wamesimama naye, Musa na Eliya, wakiongea na kumwambia juu ya kifo chake atakachokipata Yerusalemu." Eliya alionyeshwa kuwa mbinguni, Musa alikufa na kuzikwa, lakini katika Injili ya Luka, waliongea na Yesu. Walikuwa na nia ya kujua kuhusu kuondoka kwa Yesu na matukio yanayotarajiwa kutokea duniani.

Bikira Maria, ambaye ni muhimu zaidi kuliko Musa na Eliya, anajua kinachoendelea duniani. Amewatokea wengi, kama ilivyo katika Fatima, Misri, Mexico, Lourdes na Rwanda, na kuwaomba watu kusali na kutubu. Ana mawasiliano ya mara kwa mara na Yesu, Baba wa Mbinguni na Roho Mtakatifu, na ndiyo sababu tunamuomba aombe kwa niaba yetu. Ni kwa njia ya uombezi wake wenye nguvu ndio maajabu yasiohesabika yametokea katika maeneo yote haya, na mengi zaidi.

Kwa kuhitimisha, Hatumuabudu Maria; sisi ni waaminifu kwake, na tunamwomba. Ana masikio ya Mwanae Yesu na Baba yake, Mungu. Ni nani bora zaidi tunapaswa kumuomba, kumwomba, au kutafuta uombezi wake? Yeye ni mtetezi wetu; yeye ni Mama Mtakatifu wetu. Tunamuabudu Mungu Baba, Mwanae Yesu, na Roho Mtakatifu. Tunamheshimu Mama yetu Mbarikiwa. Tofauti kubwa! Tunajitolea kwake kwa sababu bila yeye, hatungekuwa na Mwanae kama Mwokozi wetu! Yeye ni mama wa Bwana wetu na, kama hivyo, ni mama yetu. Tunamtukuza mama yetu daima, iwe ni mama wa kibinadamu au wa kiroho!.

Post a Comment

0 Comments