Machapisho yanayopendwa

6/recent/ticker-posts

Bikira Maria kimbilio la Wakosefu

Katika Maisha ya mwanadamu kuna nyakati tunatenda dhambi nyingi sana, mara nyingi katika hali hii tunakosa matumaini na kujiona kama tayari tumepotea hatuwezi kuokolewa tena, kwa sababu tunaamini dhambi zetu ni kubwa sana kuliko huruma ya mwenyezi Mungu, hali hii hupelekea kuishi katika Maisha ya kukata tamaa, kujichukia na huzuni kila mara. Hali hii inatufanya wakati mwingine kuogopa hata Kwenda kuungama dhambi zetu. Basi mpendwa usikate tamaa kabisa nafahamu unaweza kuwa upo katika hali hiyo ya dhambi pengine ni ndugu au rafiki wa karibu anapitia katika hali hii. Katika nyakati hizo tunauhitaji wa msaada kutusaidia kutupa ujasiri wa Kwenda kufanya maungamo ili kurudi tena kuwa Mwana wa Mungu. Mama Maria atakuwa msaada mkubwa katika hali hii kwani yeye ni kimbilio la wakosefu.


Bikira Maria



Bikira Maria alimtokea Mt. Brigita na kumweleza kuwa, Yeye (Bikira Maria) sio tu mama wa wenye haki na wasio na hatia bali pia ni Mama wa wadhambi wanaotaka kutubu dhambi zao. Katika hali ya dhambi Maria kama mama yetu anatupokea anatukumbatia na kutusaidia kurudi kwa Mungu.

Katika kitabu cha mwanzo tunaona “Mungu aliumba mianga miwili mikubwa, mkubwa utawale mchana na ule mdogo utawale usiku” Mwanzo 1:16. Mwanga mkubwa ni jua na mwanga mdogo ni mwezi. Mababa wengi wanaeleza kuwa Mwanga mkubwa unamuakilisha Kristo anayetawala juu ya wenye haki na ule mdogo unamwakilisha Mama Maria anayewaangaza wale waishio katika giza nene la dhambi. Kwahiyo mama Maria anatuandaa katika giza la dhambi zetu, anatuandaa vema kabisa ili kunapokucha tuweze kuwa tayari kuupokea Mwanga wa Kristo atawalaye wenye haki.  Katika kueleza hili Papa Innocent III aliandika kwa kusema “yeyote aliyekatika usiku wa dhambi, basi aelekeze macho yake kwa mwezi na kumuita Maria”. Tunapotenda dhambi tunapoteza  neema ya mwanga wa haki, basi tumkimbilie Mama Maria.

Ndugu yangu ni muhimu kukumbuka kuwa Bikira Maria ni kama Safina la Nuhu ambalo ndani yake waliingia kila aina ya Wanyama ili kupata ulinzi dhidi ya gharika ya Mungu, basi ni katika kivuli hiki Mama Maria naye ni kama Safina anapokea na kuwalinda wadhambi wote wa kila aina dhidi ya adhabu ya Mungu.

Kwa kumkimbilia mama Bikira Maria utapata neema ya kutubu dhambi zako na kuziacha kabisa. Mkimbilie mama huyu pale unapoanguka, Mama huyu ni mama bora kamwe hamchoki mtu kwani sisi ni wanae, daima yupo tayari kutusaidia katika nyakati zetu za shida hasa dhambi.

Unapotokea umetenda dhambi mkimbilie, Sali kwake hasa Rozari Takatifu muombe akupe neema ya kuacha dhambi na kupata nguvu ya Kwenda kuungama, tunahitaji neema ili kukubali kukiri dhambi zetu kwa sababu kwa asili tendo la kuungama linahitaji ujasiri mkubwa, basi Mama Maria kwake utapata ujasiri na neema ya kuacha dhambi kupitia maombezi yake.

Daima unapokuwa katika hali ya dhambi kumbuka maneno haya ya Bikira Maria kwa  Mtakatifu Brigita “haijalishi ni dhambi kiasi gani mtu ametenda, daima nipo tayari kupokea haraka mtu huyo.... siangalii wingi wa dhambi alizonazo, bali nia yake ya kutubu, sisiti kumbariki na kuponya madonda ya dhambi, kwani ninaitwa na ni ndivyo ilivyo , MAMA WA HURUMA”.

Post a Comment

0 Comments